Wizara ya afya nchini Angola, imesema mlipuko wa ugonjwa wa kipindupindu nchini humo umewaua watu 108 tangu ulipozuka mapema mwaka huu.
Taarifa ya Wizara hiyo imesema ugonjwa huo unaendelea kusambaa, huku vifo vikiongezeka katika siku chache zilizopita katika baadhi ya maeneo.
Taifa hilo la Afrika lenye utajiri mkubwa wa rasilimali, limekuwa likikabiliwa na viwango vya juu vya umaskini na hali duni ya usafi wa mazingira licha ya utajiri wake wa mafuta.
Mjii mkuu wa Luanda ni miongoni mwa miji iliyoathirika, ambapo watu 48 wamekufa na wengine 43 wamepoteza maisha katika jimbo jirani la Bengo.
Kipindupindu ni maambukizi makali ya utumbo ambayo huenea kupitia chakula na maji yaliyochafuliwa na bakteria mara nyingi kutoka kwenye kinyesi.
Shirika la Afya Duniani lilisema mwaka jana kuwa, vifo vitokanavyo na kipindupindu duniani kwa mwaka 2023 viliongezeka kwa asilimia 71 ikilinganishwa na mwaka uliopita.