DMP mwenyeji Mkutano Mkuu UEM 2025

Font size:

NA MWANDISHI WETU

ASKOFU Dkt. Alex Gehaz Malasusa, amesema Dayosisi ya Mashariki na Pwani imepewa heshima ya kuwa mwenyeji wa Mkutano Mkuu wa Umoja wa Kiinjili wa Kimisioni (UEM), kwa niaba ya wanachama wa umoja huo bara la Afrika kuanzia Septemba 14 hadi 19, mwaka huu, Dar es Salaam.

Katika taarifa yake kwa wanahabari, Askofu Dkt. Malasusa ameeleza kuwa, Washarika wote wanaalikwa katika Ibada ya ufunguzi rasmi wa Mkutano huo, itakaofanyika Usharika wa Mbezi Beach, Jumapili ya Septemba 14 kuanzia saa 7.00 mchana.

“Wapendwa watu wa Mungu UEM inatokana na kazi ya Misheni ya Rhenish, Misheni ya Betheli na Misheni ya Zaire. Washiriki wa UEM leo ni makanisa ya Kiprotestanti Barani Afrika, Asia na Ujerumani, ambayo yamekuwa yakifanya kazi pamoja kwa usawa tangu 1996.
“Wanachama wa UEM wako Ujerumani, Asia (Indonesia, Ufilipino, Hong Kong na Sri Lanka) na Afrika ni nchi za Botswana, Namibia, Afrika Kusini, Cameroon, DRC, Rwanda na Tanzania,” alisema Askofu Malasusa.

Alisisitiza kuwa, UEM inatafsiri uelewa wake katika maeneo matano ambayo ni Maendeleo, Uinjilisti, Utetezi, Diakonia na Udugu (Partnership) na kuongeza kuwa, katika siku ya ufunguzi Kanisa limewaalika viongozi wa serikali na taasisi za serikali na mabalozi wote kutoka katika nchi wanachama wa UEM na wadau wote wa CCT na vyama vya kiinjili nje na ndani ya nchi.

Kaulimbiu ya Mkutano Mkuu wa UEM wa 2025 ni: Boriti Katika Jicho Letu Ubaguzi katika Kanisa na Udiakonia.  Mkazo ukiwa ni tafakuri ya kujichambua kutoka kwa makanisa na watu binafsi, ili kutambua utu wa mwanadamu na kuondoa mitazamo ya kibaguzi yenye fahamu na isiyo na fahamu na vizuizi vya kimfumo ili kuhakikisha kwamba huduma ya diakonia inafanyakazi na kupatikana kwa jamii nzima.

Mkazo huo unaakisi kuwa, Makanisa ni ya uwazi, ya haki, ya ukarimu na yanajumuisha watu wote, yakihakikisha kwamba jumuiya zilizo hatarini hazipuuzwi bali zinakuwa wapokeaji wa huduma ya diakonia, kuelimisha jamii dhidi ya ubaguzi na kukuza mazingira ambapo watu wanaohisi kubaguliwa kwa sababu ya rangi, jinsia, ulemavu wanahakikishiwa usalama, heshima na wanapewa huduma wanazostahili.

“Wapendwa watu wa Mungu, ni imani yangu kuwa mtaombea Mkutano Mkuu huu na kushiriki katika siku ya ufunguzi.
“Ahimidiwe Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo, ambaye ametubariki kwa baraka zote za kiroho na kimwili (Efe 1:3-4),” alisema Askofu Malasusa.

or

For faster login or register use your social account.

Connect with Facebook