NA
WILLIAM SHECHAMBO, Nachingwea
NI
zaidi ya miongo mitatu sasa Tanzania imekuwa katika mjadala wa namna ya
kudhibiti ndoa za utotoni ambazo bado zinashamiri katika baadhi ya mikoa, hususani
maeneo ya vijijini.
Wakati
mapambano hayo yakiendelea, Sheria ya Ndoa ya Mwaka 1971 bado inatoa uhuru kwa
msichana mwenye umri wa miaka 14 na mvulana mwenye miaka 18, kuolewa na kuoa.
Sintofahamu inatokea.
Sheria
hiyo inaleta mkanganyiko na kuwavuruga zaidi watu wa kawaida katika jamii,
ambao wanahitaji kujitosa katika mapambano ya kukomesha ndoa za utotoni.
Wakati
Sheria ya Mtoto ya mwaka 2009 inaeleza bayana kwamba mtoto ni mtu mwenye umri
chini ya miaka 18, na kwa msingi huo kisheria mtoto hana maamuzi yake binafsi,
sheria ya ndoa ya mwaka 1971 inafungua ‘uchochoro’ wa kuozesha watoto.
Ingawa
Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania haitamki mahususi umri wa mtoto, mbali
tu ya kutaja sifa za raia kuruhusiwa kupiga kura kuwa ni umri wa miaka 18, kwa
maana hiyo inatoa mwelekeo kwamba umri wa mtu kujiamulia mambo yake mwenyewe ni
miaka 18.
Kwa
mantiki hiyo, sheria inayoruhusu msichana wa umri wa miaka 14 kuolewa
inaonekana kukinzana kimantiki kuwa na umri mpevu wa mtu kufanya maamuzi
yanayohusu maisha yake, ambao kisheria unatambuliwa kama miaka 18 kwa mujibu sheria
ya mtoto ya mwaka 2009.
Sheria
ya ndoa ilifanyiwa mabadiliko mwaka 2019 na yaligusa masuala ya kugawana mali
baina ya wanandoa katika talaka, hata hivyo mabadiliko hayo hayakugusa
kipengele cha umri wa msichana kuolewa, jambo ambalo linakoleza mjadala wa
wadau wa sheria, watetezi wa haki za kijinsia na wanaharakati wa haki za
binadamu kwa ujumla.
Baadhi
ya wanaharakati wamewahi kupeleka shauri mahakamani kupinga umri wa msichana
kuolewa kuomba mahakama ibatilishe umri huo, mahakama iliagiza serikali kufanya
hivyo, hata hivyo hakuna mabadiliko yoyote yaliyofanyika mpaka sasa.
Mfano
mzuri ni shauri la Rebeca Gyumi dhidi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kuhusu
umri wa msichana kuolewa. Mahakama iliamua kuwa Serikali ichukue hatua ndani ya
mwaka mmoja kubadilisha vifungu vya 13 na 17 vya Sheria ya ndoa ambavyo
vilikuwa vinabagua kati ya mtoto wa kike na wa kiume kuingia katika ndoa.
Vigungu hivyo vinataja umri wa msichana kuolewa kuwa ni miaka 15, wakati
mvulana ni miaka 18.
Kimantiki,
vifungu vya 13 na 17 vya Sheria ya Ndoa ya mwaka 1971 vinakinzana na sheria ya
Mtoto ya Mwaka 2009; Sheria ya Elimu ya mwaka 1978 na marekesbisho yake yote,
mikataba mbalimbali kuhusu haki za watoto ambazo Tanzania imeridhia kama
mkataba wa Kimataifa wa Haki za Watoto (UNCRC) na hata Katiba ya Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, kote huko umri wa mtoto unafafanuliwa kuwa ni chini ya
miaka 18.
Kutokana
na hali hiyo, Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), ambalo kwa
takwimu za hivi karibuni lina waumini 8,500,000 na kulifanya kuwa la tatu
duniani kwa madhehebu ya Lutherani nyuma ya Ujerumani na Ethiopia, limejitosa
kusaidia juhudi za kukomesha ndoa za utotoni.
Kupitia
mradi wake wa ‘Hakuna Marefu yasiyo na mwisho’, KKKT inatekeleza kwa vitendo
wajibu wake wa kuwafundisha waumini habari za Kristo na ulimwengu ujao na
maisha ya hapa duniani ambayo yanampendeza Mungu kwa kupinga vitendo vya unyanyasaji
na ukatili wa kijinsia baina ya wanadamu.
Utafiti
uliofanywa na shirika la Twaweza mwaka 2023 ulionyesha kwamba mkoa wa Lindi ni
wa tano nchini kati ya mikoa yenye viwango vya juu vya ndoa za utotoni nchini
ukiwa na asilimia na 48. Kinara wa ndoa hizi ni Shinyanga wenye asilimia 59,
Tabora asilimia 58, Mara asilimia 55 na Dodoma asilimia 51.
Mkuu
wa Mkoa
Mkuu
wa Mkoa wa Lindi, Zeinab Telack, amesema kuwa kwa mwaka 2024 ndani ya mkoa huo,
jumla ya watoto 7,840 wenye umri kati ya miaka 10 hadi 19, wamepata mimba na
kukatisha masomo, jambo ambalo halikubaliki katika jamii na serikali kwa
ujumla.
Kwa
mujibu wa Mkuu wa Mkoa, kati ya hao 7,840 wenye umri wa kati ya miaka 10-14 ni
93 na wenye umri wa miaka 15-19 ni 7,745.
Watuhumiwa
walionaswa kuhusika na uhalifu huo, amesema wameshughulikiwa kwa mujibu wa
sheria na wengine wanaendelea kutafutwa kwa utaratibu wa kawaida wa upelelezi
katika wilaya zote za mkoa wa Lindi.
Mkuu
wa Wilaya
Naye
Mkuu wa Wilaya ya Nachingwea, Mohamed Hassan Moyo, anasema katika wilaya hiyo
vita dhidi ya ndoa za utotoni na mimba za utotoni inakwenda sambamba, na
matokeo yake ni mazuri ikilinganishwa na hali ilivyokuwa awali.
Anasema
maeneo ya katikati ya mji, ukatili wa kijinsia unaosababisha ndoa za utotoni
unaendelea kutoweka, hivyo nguvu kubwa inaelekezwa katika elimu kwa umma
unaoishi kwenye kata zilizo pembezoni ambazo zinaonekana kuwa za vijijini.
Anasema
hatua iliyofanyika ni kutoa elimu endelevu kwa jamii kuthamini elimu, kutumia
nyumba za dini kutangaza umuhimu wa malezi bora ya watoto na kufuatilia kwa
ukaribu mwenendo wa wanafunzi wanaofaulu elimu ya sekondari na idadi sahihi
wanaokwenda shuleni.
“Mimba
za utotoni bado zipo na hii inatokea kwa wale wasichana wachache wanaojihusisha
na vitendo vya ngono wakiwa bado wadogo,” anasema.
Moyo
anasema, wanaendelea kukusanya taarifa kwa kushirikiana na wenyeviti wa
serikali za mitaa, kujua hali halisi ya sasa baada ya kazi kubwa iliyofanyika
na vitengo mbalimbali vya serikali na wadau.
Maendeleo
ya Jamii
Mkuu
wa Idara ya Maendeleo ya Jamii, Halmashauri ya Wilaya ya Nachingwea, Stella Kategile,
akizungumza na gazeti la Upendo amesema wamefanikiwa kutoa elimu kwa jamii, wakiwamo
wazazi na wanafunzi wa shule za msingi na sekondari.
“Hapa
Nachingwea tumeanzisha mpango unaitwa ‘Shule Salama’, ambao una kazi kubwa ya
kutoa elimu ya kupambana na ndoa za utotoni na mimba za utotoni, tangu tuianze
imekuwa na manufaa makubwa,” anasema.
Akitoa
takwimu anasema kwa muda mfupi tangu kuanza kwa mpango huo, katika miaka mitatu
iliyopita hadi mwaka huu Februari, wamefanikiwa kuwaokoa mabinti 34 kutoka
katika mazingira ambayo yalikuwa na viashiria vya kuozeshwa wakiwa bado na umri
mdogo.
“Watoto
hawa tumewaokoa na kuwatafutia ada na vifaa vyote vinavyohitajika, hivi
ninavyozungumza nawe, wapo shuleni mikoa mbalimbali wanasoma, lakini walikuwa
tayari kwenye mipango ya kupewa waume ili waanzishe familia zao,” anasema.
Mwenyekiti
wa Kijiji
Mwenyekiti
wa Kijiji cha Nambambo, Rehema Kampela, anasema Kijiji chake ni miongoni mwa
vijiji ambavyo vimefanikiwa kupambana na mila potofu za kuwaozesha wasichana
wakiwa bado wadogo.
Alisema
kwa miaka ya nyuma, kulikuwa na utamaduni huo, lakini sasa baada ya kujengwa
kwa shule ya kisasa ya Sekondari Nambambo, iliyojengwa kwa fedha za UVIKO-19,
Watoto wakimaliza shule ya msingi wanaendelea na masomo.
“Umbali
wa shule, elimu duni kwa wazazi na walezi viliturudisha nyuma katika hili suala
unalolisema, lakini sasa tunashukuru watu wanaelimika wanajua umuhimu wa elimu
kwa watoto wao,” alisema.
Jeshi
la Polisi
Takwimu
za Jeshi la Polisi Nachingwea zinaonyesha kupungua kwa mashauri ya ukatili wa
kijinsia. Mathalani, matukio yanayowafikia yanahusu mabinti wadogo walioolewa ni
kutoka mikoa mingine na jamii za wafugaji wanaoingia Nachingwea kwa malisho.
“Kwa
Nachingwea, jamii ya hapa wamebadilika sana, suala la ndoa za utotoni lipo kwa
wahamiaji tena wale wanaoingia kimagendo bila kutoa taarifa kwa serikali za
mitaa.
"Wengi
wa hawa si wakazi wa Nachingwea na wanaishi porini sana kwa kuhamahama, hivyo
binti mdogo akipata upenyo wa kukimbia madhila ya ile ndoa anatokea kwa jamii
na kusaidiwa kufika kwetu," alisema Mkuu wa Dawati la Jinsia Nachingwea,
Asha Mponda.
Alisema
hivi karibuni, walifanikiwa kuwarejesha mabinti watatu makwao baada ya
kufanikiwa kutoroka kwa watu wazima waliowaoa na kuanza kuzunguka nao na
mifugo, harakati za kuwatafuta zinaendelea licha ya kwamba ni jamii za
wanaohamahama na mifugo.
Wananchi
Wanawake
wa Nachingwea waliozungumza na gazeti hili katika Maadhimisho ya Siku ya
Wanawake Duniani mwaka huu wa 2025, wamesema bado kuna kazi kubwa katika vita
dhidi ya ndoa za utotoni kwani jamii zinaficha taarifa za matukio hayo.
Violet
Mkisi mkazi wa Nachingwea Mjini, anasema amehamia Nachingwea kikazi, lakini
haoni kama kweli matukio ya ndoa za utotoni yamekwisha bali usiri wa familia
umesababisha utulivu wakihofia mkono wa sheria.
Mkazi
mwingine wa Nachingwea Mjini, Tabu Migomba, anasema wenyeviti wa vijiji na
serikali za mitaa, wanatakiwa kuwa mstari wa mbele kuhakikisha matukio ya ndoa
za utotoni yanaripotiwa na wahusika wanakamatwa.
“Sasa
hivi na uwepo wa Mama yetu Rais Samia Suluhu madarakani, wanawake hatutaki
mchezo na mabinti zetu, ndoto za wasichana wadogo lazima zitimie na yeyote
anayecheza na mabinti kwa kuwakatisha masomo ni wajibu wa viongozi kule chini
yaani wenyeviti wa mitaa kupambana nao,” anasema.
Ni
wazi kuwa jitihada kwa ngazi ya chini zinafanyika wilayani Nachingwea, hivyo ni
wakati sasa serikali kutafuta suluhu ya kudumu ya kisheria, ikiwemo kupeleka
muswada wa mabadiliko ya sheria ya ndoa bungeni, ili kubadili kifungu cha umri
sahihi wa msichana kuolewa kutoka umri wa miaka 14 hadi 18 ili kuendana na
tafsiri ya umri wa mtoto.
Kufanya
hivyo kutasaidia kupunguza tatizo la ndoa za utotoni, kumuinua msichana kielimu
kwa kuwa itawapa muda wa kusoma badala ya kuozeshwa
katika umri mdogo.
ends